MJADALA WA MUSWADA WA MABADILIKO YA SHERIA YA KATIBA WALAZIMIKA KUSIMAMA KWA MUDA LEO BAADA KUTOKEA HALI YA KULUMBANA KWA WABUNGE



 Mjadala wa muswaada wa mabadiliko ya sheria ya katiba wa mwaka 2013 umeshindwa kuendelea bungeni baada ya kutokea hali ya kurushiana maneno ya kashfa,kejeli iliyosababisha kurushiana makonde baina ya baadhi ya wabunge wa kambi ya upinzani bungeni dhidi ya askari wa bunge  kufuatia amri ya naibu spika wa bunge Mh Job Ndugai kuwaamuru askari hao kumtoa nje kiongozi wa kambi ya upinzani nje  ya ukumbi wa bunge hatua iliyoonekana kupingwa na wabunge wote wa vyama vya upinzani  isipokuwa Mwenyekiti wa TLP Mh Augustine Lyatonga Mrema.
Mara baada ya kipindi cha maswali na majibu ya papo kwa hapo kwa Waziri mkuu na kufuatiwa na kipindi cha maswali na majibu bungeni kwa mujibu wa ratiba ya bunge ilikuwa ni zamu ya wabunge kuendelea kuchangia muswaada wa marekebisho ya sheria ya katiba wa mwaka 2013.
Hata hivyo baadhi ya wabunge wakasimama na kuomba muongozo wa spika wakiitaka serikali kuuondoa muswaada huo bungeni kwa ajili ya kurekebisha  mapungufu kadhaa  mojawapo ikidaiwa kuwa baadhi ya taasisi na hata upande wa Zanzibar haukushirikishwa kikamilifu katika utoaji wa maoni yao huku Mh Ali Hamis Seifu mbunge wa Mkoani kupitia CUF akitoa hoja ya kutaka mjadala  wa katiba uahirishwe,ambapo uamuzi wake ni ama spika akubali ama akatae au awahoji wabunge na ndipo naibu spika alipoamua kuwahoji wabunge.
Hatua hiyo haikuonekana kuwaridhisha wabunge wa kambi ya upinzania na kutaka kura zihesabiwa suala lililoafikiwa na naibu spika Job Ndugai na kutaka kura kuhesabiwa kwa mtindo wa ndio na siyo.
Baada ya kumalizika kwa zoezi hilo naibu spika Job Ndugai akalichukulia kuwa ni kielelezo cha demokrasia ya kweli na kuruhusu wabunge kuendelea kuchangia na kumpa fursa Mh Augustine Lyatonga Mrema mbunge wa Vunjo na ndipo akasimama kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni kutaka kuzungumza huku akizuiwa na naibu spika.
Kitendo cha kuamuru askari kumtoa nje Mh Mbowe kikasababisha vurugu kubwa baina ya wabunge wa vyama vya upinzani waliokuwa wakipinga Mh Mbowe kutolewa nje dhidi ya askari wa bunge na jambo lililosababisha waziri mkuu Mh Mizengo Pinda kushindwa kushuhudia na kuamua kutoka nje .
Wakati wakitoka nje ya bunge,nje ya bunge Mh Joseph Mbilinyi akadai kupigwa teke la uso na mmoja wa askari wa bunge na kutaka kumlipizia kisha kuzuiwa na baadhi ya wabunge wenzie na kuondoka katika viwanja vya bunge akiwa ndani ya gari la kiongozi wa kambi rasmi ya upinzani bungeni Mh Freeman mbowe.
Kitendo cha wabunge hao kutoka nje ya bunge hakikumzuia naibu spika Mh Job Ndugai kuruhusu wabunge kuendelea na mjadala kama kawaida na kumpa fursa Mh Augustine Lyatonga Mrema na kutangaza kuwasamehe wabunge hao wa upinzani.

Comments

Popular posts from this blog

TUMIA SMS HIZI KUBORESHA PENZI LENU

FAIDA TISA ZA MBEGU ZA MABOGA KATIKA MWILI WA BINADAMU

NINI MAANA YA MAPENZI