VITA YA WATANI WA JADI J'PILI

KESHOKUTWA Jumapili litapatikana jibu la nani mbabe katika mechi ya kwanza ya Ligi Kuu Bara ambayo itawakutanisha watani wa jadi, msimu huu.
Simba watakuwa wenyeji wa Yanga, kila upande utakuwa unacheza mechi yake ya tisa ya ligi hiyo msimu huu, huku mabingwa watetezi wakionekana kupania kupanda na Simba kutaka kujichimbia zaidi kileleni.
Simba ina pointi 18 kileleni wakati Yanga ina 15 katika nafasi ya nne, iwapo Simba itateleza basi zitalingana pointi.
Takwimu zinaonyesha Simba inafanya vizuri zaidi hadi sasa lakini zile za uzoefu wa mechi za watani, Yanga wanaonekana kuwa na kikosi imara zaidi. Inaonyesha lazima ‘mtu atakaa’, lakini si rahisi kung’amua ni yupi.

Safu ya ulinzi:
Safu ya ulinzi ya Yanga inaonekana ni maarufu na kubwa zaidi kwa maana ya kuwa na wachezaji wazoefu zaidi na waliocheza pamoja kwa kipindi kirefu, mfano Athumani Iddi ‘Chuji’, Kelvin Yondani na Nadir Haroub ‘Cannavaro’.
Uzoefu wa Mbuyu Twite na ubora wa David Luhende lakini ndiyo imeruhusu mabao nane katika mechi nane ikiwa ni wastani wa kufungwa bao moja kila mechi wakati safu ya ulinzi ya Simba imeruhusu mabao matano.
Tofauti ya mabao matatu ni kubwa na inaonekana Joseph Owino na Gilbert Kaze ‘Demunga’ wanaanza kuelewana kiasi fulani ingawa kumekuwa na makosa mengi mara kadhaa. Hakuna ubishi, Simba watalazimika kumrudisha Issa Rashid ‘Baba Ubaya’ upande wa kushoto kwa kuwa kumeyumba.

Kiungo:
Kila upande kuna viungo bora, lakini kwa Yanga ni wazoefu zaidi, hasa Chuji au Frank Domayo kwenye ulinzi, Haruna Niyonzima katika ushambuliaji. Hata hivyo bado hawajatengeneza mambo bora zaidi katika mechi nane za mwanzo.
Kwa upande wa Simba inaonekana Jonas Mkude amekaa vizuri katika namba sita, lakini namba nane bado haijapata mwenyewe, kwani wakati mwingine Abdulhalim Humud au  kinda mwenye kipaji, Said Ndemla, ambaye hata hivyo anabadilishwa mara kwa mara, lazima wajipange.
Kwa pembeni, Yanga wana watu wenye kasi kama Simon Msuva na Kocha Ernie Brandts kama ataamua kumchezesha Mrisho Ngassa pembeni. Lakini Simba pia wako sawa, Haruna Chanongo ni hatari na ana uwezo wa kupiga mashuti makali na kulia ni Amri Kiemba au Ramadhani Singano ingawa bado haina uhakika nani ataanza.

Washambuliaji:
Kwa takwimu, safu ya ulinzi ya Simba ni kali zaidi kwa kuwa ina mabao 18, mengi zaidi ya Yanga yenye 15 na tegemeo ni Mrundi, Amissi Tambwe, aliyefunga manane na wamepanga kumbana vilivyo.
Betram Mwombeki wa Simba na Didier Kavumbagu wa Yanga watakuwa kivutio na tatizo kwa mabeki, lakini kasi ya Ngassa, ujanja wa Tambwe ni mambo muhimu ya kuangalia na yatawasumbua walinzi wa kila upande.
Mechi nne za mwisho:
SIMBA:- Katika mechi zake nne za mwisho, Simba ilikusanya pointi nane baada ya kushinda mechi mbili dhidi ya Prisons na JKT Ruvu na sare mbili dhidi ya Ruvu Shooting na Mbeya City. Prisons 1-0, Ruvu Shooting 1-1, JKT 2-0, Mbeya City 2-2.

Yanga:-Katika mechi nne za mwisho, Yanga walipata pointi tisa baada ya kufungwa moja dhidi ya Azam FC na kushinda tatu dhidi ya Kagera, Mtibwa Sugar na Ruvu Shooting.
Kagera 2-1, Mtibwa 2-0, Ruvu Shooting 1-0, Azam 2-3.

Uzoefu:
Hiki ndicho kikosi Yanga wanaweza kujivunia zaidi, kwani wana kikosi kilichokaa pamoja kwa muda mrefu zaidi na wameshacheza mechi dhidi ya Simba zaidi ya mara mbili.
Upande wa Simba ni kikosi ambacho wachezaji wengi wanacheza kwa mara ya kwanza dhidi ya Yanga wakiwa na Simba. Hivyo kutakuwa na ugumu kwao lakini bado haliwezi kuwa tatizo la moja kwa moja kama watajituma.
Takwimu ni kitu bora kupima kilichotokea, lakini bado dakika 90 ya kila mechi hujitegemea ili kutengeneza takwimu mpya. Hivyo itakuwa mechi ngumu ambayo ni vigumu kutabiri mshindi.

Wenye mabao:
Simba:-Wachezaji wenye uchu wa mabao ambao hakuna ubishi wataipa Yanga shida ni Tambwe ambaye tayari ana mabao nane na ndiye anaongoza kwa upachikaji mabao hadi sasa.
Chanongo tayari ana mabao matatu, atataka kuongeza la nne na kuifunga Yanga ni kitu bora kwake, hivyo atakuwa mwiba.
Jonas Mkude, ndiye kiungo mkabaji mwenye mabao mengi zaidi msimu huu, ana matatu. Moja la penalti lakini bao moja alilofunga dhidi ya Prisons hadi sasa ndilo bora zaidi na Kocha wa Taifa Stars, Kim Poulsen amesema hata Ulaya linapatikana kwa shida.

Yanga:- Kavumbagu ndiye anaongoza mabao Yanga, ana manne na uchu wake uko juu ingawa ana tatizo la kushindwa kumalizia jirani ya lango.
Hamisi Kiiza, huyu ni hatari zaidi kwa Simba, mechi ya mwisho alifunga bao zuri katika ya msitu wa mabeki wa Simba, sasa ana mabao matatu.
Jerry Tegete anaweza asianze, lakini akipata nafasi pia ni tatizo kwa Simba hasa kwa kuwa wana makosa ya kujisahau kuondosha mipira haraka langoni mwao au kipa Abel Dhaira kutema mara kwa mara.

Vichwa:
Vichwa viwili vinaweza kuwa ni vya kuchungwa zaidi, Mwombeki ambaye ni mrefu, akipewa nafasi ya kutoa pasi za vichwa itakuwa ni tatizo kwa Yanga na Tambwe anaweza kuitumia nafasi hiyo kuwamaliza.
Kavumbagu, mzuri kwa pasi za vichwa pia kumalizia langoni mipira ya juu, Simba wanamkumbuka walipolala mabao 2-0. Hivyo lazima kuwe na mwenye uwezo wa kuruka naye juu.
SIMBA
Kocha: Abdallah Kibaden
Kocha Msaidizi:  Jamhuri Kihwelo ‘Julio’
Nahodha: Said Nassor ‘Chollo’
Kambi ilipo: Bamba Beach, Dar

YANGA
Kocha: Ernie Brandts
Kocha Msaidizi: Felix Minziro
Nahodha: Nadir Haroub ‘Cannavaro’
Kambi ilipo: Pemba, Zanzibar

Kikosi kipya:
Kama ni tathmini ya kikosi, inaonekana Simba ina nafasi ndogo ya kushinda mechi hiyo kwa kuwa mara ya mwisho timu hizo zilipokutana msimu uliopita na Simba kulala kwa mabao 2-0, kuna mabadiliko makubwa.
Simba itawakosa wachezaji muhimu sita pamoja na Kocha Patrick Liewig.
Wachezaji ni Shomari Kapombe, Mwinyi Kazimoto, Shomari Kapombe, Musa Mudde, Mrisho Ngassa aliyehamia Yanga, Felix Sunzu aliyeingia siku hiyo na nahodha Juma Kaseja aliyeachwa kwa kisingizio cha kiwango kushuka.
Hii ni dalili wazi kwamba Simba itakuwa na kikosi kipya kinachojengwa na ina wachezaji ambao kwa mara ya kwanza wanacheza mechi hiyo akiwemo kipa Abel Dhaira, Gilbert Kaze ‘Demunga’, Betram Mwombeki, Said Ndemla na Zahoro Pazi.
Yanga, kikosi chao mabadiliko ni Ngassa tu ambaye pia ni sawa amerejea nyumbani, kila mmoja alikuwepo msimu na mechi iliyopita.
Uzoefu wa mechi au kikosi kujuana vizuri ni sehemu ya kusaidia wacheze vizuri ingawa haiwezi kuwa jibu la matokeo ya keshokutwa.

Comments

Popular posts from this blog

TUMIA SMS HIZI KUBORESHA PENZI LENU

FAIDA TISA ZA MBEGU ZA MABOGA KATIKA MWILI WA BINADAMU

NINI MAANA YA MAPENZI