MZIMU WA NYERERE WAWATESA WAGOMBEA WA URAIS 2015




Kwa ufupi
Makada hao pia wamezuru kaburi la Baba wa Taifa na wengine kutumia kuaminiwa kwake na wananchi wakati akiwa na umri mdogo ili kujenga hoja kuwa uzoefu na umri si suala la kuzingatiwa katika kupata kiongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano.

 Dar es Salaam. Jina la Mwalimu Julius Kambarage Nyerere limeibuka ghafla na kwa nguvu baada ya makada wanaowania kupitishwa na CCM kuanza kutangaza nia, huku wengi wao wakionyesha kuaminiwa na muasisi huyo wa Taifa na wengine kuahidi kufuata miiko aliyoiweka wakati alipoongoza Serikali ya Awamu ya Kwanza.
Makada hao pia wamezuru kaburi la Baba wa Taifa na wengine kutumia kuaminiwa kwake na wananchi wakati akiwa na umri mdogo ili kujenga hoja kuwa uzoefu na umri si suala la kuzingatiwa katika kupata kiongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano.

Mwalimu Nyerere, aliyeongoza Tanganyika tangu mwaka 1961 na baadaye Tanzania kuanzia mwaka 1964 hadi 1985 alipong’atuka, anajulikana sana kutokana na kuanzisha Azimio la Arusha mwaka 1967 lililoweka miiko ya uongozi bora na kuweka misingi ya siasa za ujamaa, mambo ambayo yalitenguliwa na Azimio la Zanzibar miaka michache baada ya kuachia urais.
Mbali na kutangaza miiko hiyo iliyojenga maadili ya uongozi wakati nchi ikielekea kujenga Taifa la kijamaa, Mwalimu Nyerere alikuwa na nguvu ya ushawishi na mkali dhidi ya vitendo vya rushwa na ufisadi, jambo lililomfanya aheshimike ndani na nje ya nchi.
Wakati Taifa likisikiliza hoja za wanaotia nia ya kuwania urais ikiwa ni miezi michache baada ya Bunge la Katiba kuondoa mambo ya maadili kwenye Rasimu ya Katiba, suala hilo linaonekana kurudi kwa nguvu kwenye sera za wagombea uongozi ambao wanataja kila mara jina la Nyerere, miaka 16 baada ya kifo chake.
“Wanamtumia Nyerere kwa sababu wanajua alikuwa muadilifu, alikuwa akisema kitu watu wanatekeleza. Leo kiongozi anatoa maagizo hakuna anayetekeleza,” alisema mchungaji wa Kanisa la Pentekoste, Dk Damas Mukasa alipoulizwa maoni yake kuhusu kuibuka kwa jina hilo la muasisi wa Tanganyika.
Akitangaza rasmi nia ya kuutaka urais kwenye hafla iliyofanyika uwanja wa ofisi ya CCM ya Mkoa wa Lindi, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe alisema kuwa anatosha kushika wadhifa huo na kwamba Mwalimu Nyerere atafurahi huko aliko iwapo atachaguliwa kuwa Rais kwa miaka 10 ijayo.
Pia, Membe alisema kuwa Machi mwaka huu alikwenda Butiama na kuzuru kaburi la Mwalimu Nyerere ambako alipiga magoti na kumweleza nia yake ya kuutaka urais.
“Nilipiga goti nikamwambia Mwalimu, navitaka viatu vyako, alivivaa Mzee (Ali Hassan) Mwinyi, Mzee (Benjamin) Mkapa na (Rais, Jakaya) Kikwete. Sasa nataka kuvivaa mimi na nina hakika vinanitosha,” alisema Membe.
“Ninaamini vitanitosha. Nikamwambia chondechonde, kama havitanitosha, niambie… timu yangu ya mikoani ikawahi kuniambia unatosha.”
Mkurugenzi mkuu wa zamani wa Idara ya Usalama wa Taifa, Dk Hassy Kitine naye alitumia jina hilo wakati akitangaza nia ya kutaka kurejea Ikulu ambako alifanya kazi chini ya utawala wa muasisi huyo, akiahidi kutumia miaka mitano kuirudisha Tanzania ya Mwalimu Nyerere.
Dk Kitine alitumia sehemu kubwa ya hotuba yake aliyoitoa mjini Dodoma kutoa mifano ya utendaji wa Mwalimu Nyerere na kuwaponda wengine waliojitokeza kuwa hawana sifa za kumfikia.


“Ninataka kuirudisha Tanzania ya Mwalimu Nyerere… sikuwahi kutangaza wala kuonyesha dalili zaidi ya kukaa na kutafakari katika nafsi… najua sitaweza kufanya kama alivyokuwa Mwalimu, lakini nitasimamia katika misingi ya utendaji ya Mwalimu Nyerere,” alisema waziri huyo wa zamani.
“Ikulu si pa kukimbilia, Ikulu ni shida, Ikulu ni matatizo,” alisema ofisa huyo mwandamizi wa zamani wa Idara ya Usalama wa Taifa.
“Mwalimu alisema ‘ukiona mtu anakimbilia Ikulu kwa namna yoyote ile, na hasa kwa mapesa, mapesa siyo fedha, mapesa, mapesa, mapesa mpaka yanatisha. Huyu mtu akienda Ikulu lazima azirudishe, na (Ikulu) si pa biashara. Sasa anakwenda kufanya biashara gani?’
“Huyu ni wa kuogopa kama ukoma…mimi ninaijua Ikulu kuliko mgombea mwingine yeyote. Nilikuwa Ikulu kama kiongozi, kila mlango wa chumba Ikulu naujua, hata alipolala Baba wa Taifa. Ikulu si pa kukimbilia.”
Edward Lowassa, Waziri Mkuu wa zamani, hakuzungumza kitu kuhusu Nyerere akiwa Mkoani Mara ambako alikwenda kutafuta wadhamini, badala yake alilitembelea kaburi la Mwalimu Nyerere ambapo aliwasha mshumaa na kuuweka kaburini.
Pamoja na kutotumia jina la Nyerere, lakini siku aliyotangaza nia kwenye Uwanja wa Sheikh Amri mjini Arusha, mmoja wa waalikwa ambaye ni mwanasiasa mkongwe, Kingunge Ngombare Mwiru, alipopewa nafasi ya kuzungumza baada ya hotuba ya Lowassa, alisema mtiania huyo aliandaliwa na Mwalimu, ambaye alisema alikuwa akitaka wasomi na waliopitia jeshi.
Alisema Lowassa amesoma na amepitia jeshini na alikwenda kwenye vita dhidi ya majeshi ya Idd Amin wa Uganda.
Akitangaza nia ya kugombea urais, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya alisema kuwa ameamua kuelezea nia hiyo kwenye Uwanja wa Mkapa, mjini Mbeya kwa kuwa alizaliwa mkoani humo na pia Mwalimu Nyerere alikuwa akifanya mikutano eneo hilo alipokuwa katika harakati za kudai uhuru wa Tanganyika.
“Eneo hili enzi hizo lilikuwa likiitwa Welfare Center, hivyo Waafrika walikuwa wakikusanyika hapa kumsikiliza Mwalimu Nyerere,’’ alisema Profesa Mwandosya.
Alisema wapo viongozi wengi waliojitokeza kuwania nafasi hiyo huku wakimwaga fedha jambo ambalo halipaswi kufanywa na viongozi wanaotarajia kuwatumikia Watanzania kwa uadilifu.
“Wakati wa Mwalimu Nyerere rushwa ilikuwa ni adui wa haki, leo hii rushwa iko nje nje kama njugu. Wanapotoa hela zao chukueni, lakini msiwaunge mkono hawafai kuongoza nchi,” alisema Profesa Mwandosya ambaye mwaka 2005 alishika nafasi ya tatu kwenye kinyang’anyiro cha urais.
Steven Wasira, ambaye aliteuliwa kuwa waziri kwa mara ya kwanza wakati wa utawala wa Mwalimu Nyerere, hakuwa nyuma katika kutumia jina la kiongozi huyo maarufu duniani. “Mwalimu Nyerere aliwahi kuniuliza ninataka nini kati ya utajiri na kuongoza watu, alisema nikitaka utajiri nichague kuwa mfanyabiashara kwani nitanunua kwa bei rahisi na kuuza aghali,” alisema Wasira wakati akitangaza nia mjini Mwanza.


Alisema Nyerere alimweleza kuwa hawezi kuwa tajiri kwa kazi ya kutumikia watu kwa mshahara na kwamba mfanyabiashara ndiye anaweza kutajirika.

“Kwa hiyo nimewatumikia Watanzania katika nafasi mbalimbali tangu nikiwa na umri wa miaka 25, lakini sijawahi kuhusishwa na kashfa za rushwa, nyie ni mashahidi sijawahi kuhusishwa na kashfa za Epa wala Tegeta Escrow,” alisema.
Pia, Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba mwenye umri wa miaka 40, alitangaza nia yake ya kutaka kugombea urais kwenye Ukumbi wa Mwalimu Nyerere katika Chuo cha Mipango Dodoma huku akipinga hoja inayotolewa na baadhi ya watu kuwa anataka nafasi hiyo akiwa na umri mdogo.
Alisema hata Mwalimu Julius Nyerere alikuwa rais akiwa na miaka 40, tena akitoka kufundisha sekondari.

“Watu wanataka kuwatoa Watanzania katika ajenda kwa kuzungumzia vitu vyepesi. Eti wanasema ukimaliza kuwa rais wakati bado kijana utafanya nini. Nifanye nini tena wakati nitakuwa nimeshamaliza kazi. Najipambanua kwa ajenda yangu na wale watakaoniangalia wataangalia ajenda yangu,” alisema.
Haikuwa ajabu kwa jina la Mwalimu Nyerere kutajwa mjini Butiama wakati mtoto wake, Makongoro Nyerere alipokuwa akitangaza nia ya kugombea urais kwa tiketi ya CCM na lilianzia midomoni mwa Mwenyekiti wa Wilaya ya Rorya, Samwel Kiboye aliyetaka Watanzania kumuenzi Baba wa Taifa kwa kumkabidhi kijana wake fimbo ya kuongoza nchi.

“Tukimkabidhi kijana wa Baba wa Taifa viatu vya baba yake tutakuwa tumemuenzi kiuhakika Baba wa Taifa hili. Kwanza kijana huyu ni mwadilifu na pia ni kiongozi shupavu kwani mifano yake tunayo na tulishaionja wakati akiwa mwenyekiti wa mkoa huu,” alisema Kiboye.

Wananchi walonga
 Lakini watu mbalimbali walioongea na Mwananchi walikuwa na maoni tofauti kuhusu kutumiwa kwa jina hilo wakati huu wa kutafuta kiongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano.
Mratibu wa Umoja wa Wanawake Wanasiasa Tanzania (Ulingo), Dk Ave Maria Semakafu alisema watu wanaogombea urais wanalitaja jina hilo kwa sababu wamebaini kuwa wananchi wamekata tamaa kutokana na kukithiri kwa rushwa na ufisadi ambao haukuwepo wakati wa Nyerere alipoongoza Taifa kwa miaka 25.
Dk Semakafu alisema iwapo maendeleo ya Tanzania yangeenda kwa kasi iliyokuwa imeanzishwa na Baba wa Taifa, nchi ilipaswa kuwa mbali kiuchumi, lakini jambo hilo halijawezekana kutokana na baadhi ya viongozi kuvuruga misingi aliyoiweka. “Watu wachache wameibuka na ‘kubaka’ mfumo matokeo yake tumerudi nyuma kama wakati wa nchi inapata uhuru. Wakati wa Mwalimu utu ulikuwa na thamani si kama ilivyo sasa,” alisema Dk Semakafu
.
“Wanaomtaja Mwalimu Nyerere majukwaaani hawana maana kuwa wanataka kufukua mwili wake, bali wanatamani namna alivyoendesha nchi kiasi kwamba hata mwananchi wa kawaida alikuwa ananufaika na rasilimali za Taifa.”
Pia, alisema kuwa baadhi ya viongozi wanaotaka urais hivi sasa walikuwemo serikalini kwa muda mrefu, lakini walishindwa kufanya baadhi ya mambo kwa kuwa hawakuwa na mamlaka na ndiyo maana wanasema wakipewa nafasi watafanya kama alivyofanya Mwalimu Nyerere.


Katibu Mkuu wa Taasisi ya Wanazuoni wa Kiislamu, Sheikh Khamis Mataka alisema wanaokumbuka uongozi wa Mwalimu Nyerere hawakumbuki mfumo wa ukuaji wa uchumi kwa njia ya ujamaa, bali wanakumbuka namna ambavyo viongozi walikuwa na maadili.
Sheikh Mataka alisema kuwa wakati wa uongozi wa Serikali ya Awamu ya Kwanza, nchi ilikuwa ikifuata mfumo wa siasa unaoeleweka na jamii yote, tofauti na ilivyo hivi sasa ambapo haijulikani ipo kwenye mfumo wa ujamaa au ubepari.

“Hivi sasa tunaimba kijamaa tunacheza kibepari, hata wale waliokuwa wanasifiwa wakati wa ujamaa leo wamekuwa wafanyabiashara wakubwa,” alisema Sheikh Mataka na kuongeza kuwa Baba wa Taifa atakumbukwa kwa haki, maadili na utawala bora.

Mchungaji wa Kanisa la Pentekoste Agizo, Dk Damas Mukasa alisema watu wanamtaja Mwalimu Nyerere kwa sababu kuu mbili; kwanza alikuwa ni kiongozi mwenye msimamo hasa katika jambo aliloliamini na kwamba watu walikuwa wakimsikiliza na kutii maagizo aliyosema na pili, alikuwa mwadilifu.
Lakini Mwenyekiti wa Chama cha Kidemokrasia (DP), Mchungaji Christopher Mtikila alitofautiana na wengine akisema kuwa yeyote anayetamani kurudisha uongozi wa Mwalimu Nyerere, hakumjua vyema kiongozi huyo.
“Mfumo uliopo ulianzishwa na Mwalimu Nyerere. Hatuhitaji kumkumbuka mtu yeyote tunachotaka ni mabadiliko, elimu ya wakati wa ukoloni ilikuwa nzuri kuliko ya mtu anayemaliza chuo kikuu leo,” alisema Mchungaji Mtikila

Comments

Popular posts from this blog

TUMIA SMS HIZI KUBORESHA PENZI LENU

FAIDA TISA ZA MBEGU ZA MABOGA KATIKA MWILI WA BINADAMU

UMUHIMU WA KUJIFUNZA SAIKOLOJIA