PENZI LISILOISHA 3

Jafet, kijana mdogo ambaye alikuwa amehitimu darasa la saba na kufaulu vizuri kuendelea na masomo ya sekondari, anajikuta akikwama kuendelea na shule kutokana na ufukara wa kupindukia wa wazazi wake. Hali hiyo inamuumiza sana Jafet hasa anapoona wenzake wameanza kwenda shule, muda wote anashinda akiwa analia na kujiinamia kwa huzuni.
Mama yake aliyekuwa akijishughulisha na kazi ya kufanya vibarua vya kupalilia mashamba ya mihogo ili apate chakula cha yeye na familia yake, naye anaumizwa sana na hali aliyokuwa nayo mwanaye. Baada ya kumlalamikia na kumlilia sana, mwanamke huyo maskini anaamua kumsaidia mwanaye.
Kama miujiza, anapata habari za mapadri waliokuwa wanasaidia kuwasomesha watoto waliofaulu kutoka kwenye familia za kimaskini. Hatimaye ndoto ya Jafet ya kuendelea na masomo iliyokuwa imefifia, inang’ara upya baada ya mapadri kukubali kumsomesha. Anapelekwa Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Mtakatifu Paulo iliyopo Kwimba, Mwanza anakoyaanza masomo.
Siku zinasonga mbele, Jafet anaanza kubadilikia kimwili na kuwa mkubwa. Ni katika kipindi hicho ndipo anapoanza kusumbuliwa na hisia za kimapenzi na kutamani kuwa na msichana.
Je, nini kitafuatia? 
Mambo!”
“Poa.”
“Unaitwa nani mwenzangu maana leo siyo mara ya kwanza tunakutana.”

“Sitakutajia jina langu ila nasoma Shule ya Wasichana ya Bwiru,” alisema msichana ambaye Jafet alikutana naye jirani na duka la madawa ya mifugo, akiwa ameagizwa shuleni kwao kwani alikuwa akihusika na kitengo cha miradi ya shule.
Kiumri hawakuwa wamepishana sana na Jafet, mtoto wa kiume akaanza kushusha ‘mistari’ kwa kujaribu kumvuta karibu msichana huyo kimaongezi kwani alishatokea kumpenda sana, akaona huo ndiyo muda muafaka wa kumueleza kilichokuwa ndani ya moyo wake.
Mazungumzo kati ya wawili hao yaliendelea huku muda mwingi msichana huyo mrembo, akichekacheka na kung’ata vidole.
Japokuwa Jafet hakuwahi kutongoza hata siku moja kwenye maisha yake, siku hiyo alijikuta akipata ujasiri wa hali ya juu, akawa anamtazama msichana huyo usoni bila aibu na kuendelea kumsemesha mambo mbalimbali.
Ungewaona jinsi walivyokuwa wakizungumza, usingepata shida kuelewa kwamba walikuwa wanatongozana kutokana na jinsi msichana huyo alivyokuwa anahangaika, mara achume majani, mara akate maua au ang’ate kucha, ilikuwa vituko vitupu.
“Mimi naitwa Jafet Lubongeja, nasoma Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Mtakatifu Paulo iliyopo Kwimba, Mwanza. Niambie basi na wewe jina lako, tafadhali nipo chini ya miguu yako,” Jafet alikuwa akimbembeleza msichana huyo, hatimaye akamwambia kwamba anaitwa Anna Kamazima.
“Whaoo! Jina zuri kama wewe mwenyewe ulivyo.”
“Kwani mi mzuri?” alisema msichana huyo kwa aibu za kikekike, Jafet akaendelea kumwagia sifa lukuki, hatimaye akamueleza kilichokuwa ndani ya moyo wake. Kabla hajajibiwa, mlio wa simu ulianza kusikika.
Msichana huyo akaingiza mkono kwenye kibegi chake kidogo alichokuwa amekibeba na kutoa simu nzuri ya kisasa, Jafet akabaki amepigwa na butwaa kwani hakutegemea kama msichana mdogo kama huyo anaweza kuwa na simu ya gharama kubwa kiasi hicho.
“Haloo shikamoo baba,” alisema Anna huku akisogea pembeni kuzungumza na simu hiyo, akawa anamuelekeza sehemu alipo kisha akakata simu.
“Samahani tutaongea siku nyingine baba yangu ananifuata, nimemuelekeza nilipo,” alisema msichana huyo mdogo lakini mrembo huku akionesha kuwa na haraka. Licha ya Jafet kumbembeleza ampe jibu lake, aliendelea kumsisitiza kuwa aondoke eneo hilo kwani hatapenda baba yake amkute na mvulana wakati anajua kwamba anasoma shule ya wasichana tupu.
Hatimaye Jafet aliondoka kwa shingo upande, akaenda kununua dawa za mifugo ya shuleni kwao kama alivyoagizwa. Akiwa anajiandaa kuondoka, alisikia muungurumo wa gari likija jirani na duka lile upande aliomuacha Anna, akageuka na kulitazama gari hilo na kujikuta akipigwa na mshangao.
Lilikuwa ni gari zuri sana ambalo hakuwahi kuliona katika maisha yake, hasa ukizingatia kwamba kipindi kirefu alikuwa akiishi kijijini kwao, Rwamgasa ambako hakukuwa na mtu mwenye gari.
Akiwa anaendelea kulishangaa gari hilo kwa jinsi lilivyokuwa zuri, aliliona likisimama jirani na lile duka, mwanaume wa makamo akateremka na kuanza kuangaza macho huku na kule.
“Daaad!” (Babaaaa) ilisikika sauti ambayo Jafet hakupata tabu kuigundua kuwa ni ya msichana aliyekuwa akizungumza naye muda mfupi uliopita, Anna. Akamuona msichana huyo akiinuka kwa kasi sehemu aliyokuwa amekaa na kumkimbilia mwanaume huyo, akamkumbatia kwa furaha kisha wote wakaelekea kwenye gari.
“Yule ndiyo baba yake? Mbona wamefanana sana?” Jafet alijisemea moyoni huku akiwa bado amepigwa na butwaa. Hakuhitaji ufafanuzi zaidi kwani mwanaume huyo alikuwa amefanana sana na Anna, akajua moja kwa moja ndiyo baba yake.
Kwa jinsi Jafet alivyokuwa anazungumza na Anna muda mfupi uliopita, hakudhani msichana huyo anaweza kuwa anatokea kwenye familia ya kitajiri kiasi hicho kwani hakumuoneshea maringo yoyote kama ambavyo alizoea kusikia kwamba wasichana wanaotoka familia za kitajiri wanaringa sana.
Akiwa bado anashangaa, lile gari lilianza kuondoka taratibu huku wawili hao wakionekana kuzama kwenye mazungumzo. Kitendo hicho kilionesha kumkatisha mno tamaa kwa kuamini ombi lake haliwezi kukubaliwa kwani kulikuwa na tofauti kubwa ya kimaisha kati ya wawili hao.
Kila alipokumbuka umaskini wa kutupwa aliouacha nyumbani kwao, Rwamgasa, familia yao ikiishi kwenye kibanda kidogo cha udongo na nyasi, jinsi wazazi wake walivyokuwa mafukara, alijiona hana hadhi hata ya kumsogelea msichana huyo.
Akaondoka kuelekea shuleni kwao huku akiwa mnyonge sana, mawazo mengi yakiendelea kupita ndani ya kichwa chake, muda mwingine akiwalaumu wazazi wake kwa kushindwa kuyapatia maisha kama watu wengine.
Alifika shuleni kwao, Sekondari ya Wavulana ya Mtakatifu Paulo lakini tofauti na siku zote, alionesha kuwa mnyonge sana. Akakabidhi vifaa alivyotumwa kuvinunua kisha akaenda bwenini kwao na kujilaza kitandani, mawazo mengi yakiendelea kupita ndani ya kichwa chake kuhusu Anna, msichana aliyetokea kuuteka moyo wake ghafla. Kila alipokuwa anamfikiria, aliona kabisa uwezekano wa kuwa naye haupo, akawa anaendelea kuteseka ndani ya moyo wake.
Siku hiyo ilipita, Jafet akawa anaendelea kusoma kwa bidii kama ilivyo kawaida yake huku mawazo ya Anna yakiendelea kukisumbua kichwa chake. Siku moja akiwa darasani akiendelea na masomo yake, karani wa shule hiyo alikuja kumwita.
“Wewe ndiyo Jafet Lubongeja?”
“Ndiyo.”
“Kuna barua yako ofisini, twende ukaichukue,” alisema karani huyo na kuongozana na Jafet mpaka kwenye ofisi yake ambapo alimtolea bahasha kubwa ya khaki iliyokuwa imeandikwa jina lake kwa mwandiko mzuri, ikiwa imebandikwa stempu kuonesha kuwa imetumwa kwa njia ya posta.
Jafet aliipokea na kusaini kwenye kitabu maalum huku akiendelea kujiuliza maswali yaliyokosa majibu kuhusu barua hiyo. Hakuwahi kutumiwa barua kwa njia ya posta hata siku moja, akawa na shauku kubwa ya kutaka kujua ni nani aliyemtumia.
Hakwenda tena darasani, badala yake alienda moja kwa moja bwenini na alipoingia tu, aliifungua bahasha hiyo kwa umakini. Akakutana na bahasha nyingine ndani iliyokuwa na mauamaua mazuri, akaitoa na kuifungua.
Alichokiona kilimfanya asiyaamini macho yake, kulikuwa na kadi nzuri iliyokuwa imepuliziwa manukato mazuri, akaitoa huku uso wake ukiwa umejawa na tabasamu na kuifungua ndani

Comments

Popular posts from this blog

TUMIA SMS HIZI KUBORESHA PENZI LENU

FAIDA TISA ZA MBEGU ZA MABOGA KATIKA MWILI WA BINADAMU

UMUHIMU WA KUJIFUNZA SAIKOLOJIA