LOVE STORY5

Ebola, ugonjwa hatari usio na tiba wala kinga, unaikumba Liberia, nchi iliyopo Magharibi mwa Bara la Afrika na kusababisha maafa makubwa kwa wananchi wake. Watu wengi wanaambukizwa ugonjwa huo na ndani ya muda mfupi tu, mamia ya wananchi wanapoteza maisha.
Licha ya serikali kujitahidi kwa kadiri ya uwezo wake kupambana na ugonjwa huo, kazi inakuwa ngumu na maelfu ya watu wanaendelea kupoteza maisha na kuambukizwa ugonjwa huo hatari.Hali inazidi kuwa tete kadiri siku zinavyozidi kusonga mbele, maiti nyingi za watu waliokufa kwa ugonjwa huo zinatapakaa mitaani huku maelfu ya wakazi wakiyakimbia makazi yao wakiogopa kuambukizwa ugonjwa huo hatari.
Jiji la Monrovia linabaki kuwa kimya kabisa huku harufu za maiti zikizidi kuifanya hali kuwa ya kutisha mno. Mitaa yote inakuwa kimya kabisa, kelele pekee zinazosikika ni za mbwa wanaogombea mizoga ya watu waliokufa kwa ugonjwa huo.
Ndani ya nyumba moja, watu wawili waliokuwa wapenzi wanasikika wakibishana. Mwanaume anamtaka mpenzi wake aondoke na kurudi nchini kwao, Sangabuye ili asije akaambukizwa ugonjwa huo lakini mwanamke anakataa akitaka waondoke pamoja au wabaki wote na kufa pamoja.
Upande wa pili, historia ya nchi ya Sangabuye inaelezewa ambapo Rais Martin Wela anaingia madarakani baada ya serikali iliyokuwepo kupinduliwa na jeshi. Muda mfupi baadaye anamuoa mpenzi wake wa siku nyingi, Sophia Marcel na baada ya miezi tisa, ndoa yao inajibu ambapo wanapata mtoto mzuri wa kiume, jambo linaloongeza furaha kwenye familia hiyo.
Rais Martin Wela anaendelea kuwatumikia wananchi wa Sangabuye na sasa yupo kwenye mchakato wa kuibadilisha serikali ya kijeshi kwenda kwenye demokrasia ya kweli.
Je, nini kitafuatia?

Licha ya Rais Martin Wela kuonesha nia ya kutogombea tena kwenye uchaguzi wa kidemokrasia, shinikizo kutoka kwa wananchi na viongozi wa juu wa jeshi ambao ndiyo waliomuweka madarakani lilikuwa kubwa mno kiasi kwamba akawa hana ujanja zaidi ya kukubaliana na matakwa ya wengi.
Ikabidi afanye kama alivyokuwa ameelekezwa, mchakato wa kuunda serikali ya kidemokrasia ukaanza ambapo vyama mbalimbali vya siasa vilianza kusajiliwa upya. Martin Wela akaunda Chama cha Sangabuye Alliance for Democracy and Transparency (SADT).
Muda mfupi tu tangu kuanzishwa kwake, chama hicho kilipata umaarufu mkubwa huku wananchi wengi wakijiunga nacho kumfuata Rais Martin Wela, kipenzi na chaguo la wengi. Kama ulivyo utaratibu wa serikali za kiraia, vikao vya ndani vya kila chama vilianza kufanyika kwa lengo la kila kimoja kujiwekea sera zake, ilani na kuteua wagombea katika ngazi mbalimbali.
Kama ilivyotarajiwa na wengi, Chama cha SADT kilimteua Rais Martin Wela kuwa mgombea wake wa urais huku akipewa pia jukumu la kuteua vijana alioona wanafaa kugombea nafasi za ubunge katika majimbo yote ya uchaguzi.
Kwa kuwa Rais Martin alikuwa mwanaharakati kwa kipindi kirefu kabla hajapewa nafasi ya kuiongoza nchi hiyo, alikuwa akiwajua vizuri vijana wenye uchungu na nchi yao. Kwa kuwa alipewa nafasi ya upendeleo ya kuteua wagombea wa nafasi za ubunge ambao aliona wanafaa, aliifanya kazi hiyo kwa uadilifu wa hali ya juu, akawateua vijana waliokuwa na sifa zote za kuwa viongozi bila upendeleo wa aina yoyote.
Tume huru ya uchaguzi nayo iliundwa na kupewa jukumu la kuandaa na kusimamia uchaguzi huo ambao ulipangwa kuwa huru na wa haki. Maandalizi yaliendelea kufanyika huku familia ya Martin Wela nayo ikizidi kuwa na furaha.
Mtoto Charles akawa anaongezeka ukubwa na akili kadiri siku zilivyokuwa zinasonga mbele. Hatimaye tume ya uchaguzi iliyoundwa, ikatangaza kuanza rasmi kwa kampeni za kuelekea kwenye uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani.
Japokuwa kulikuwa na vyama zaidi ya kumi na mbili, vikiwa na wagombea wenye sifa tofautitofauti katika ngazi zote, Alliance for Democracy and Transparency (SADT) kilichokuwa kinaongozwa na Rais Martin Wela kilionekana kuwa na mvuto mkubwa kwa wananchi.
Katika mikutano ya kampeni ya chama hicho, idadi kubwa ya watu walikuwa wakihudhuria na kuwashangilia wagombea wa nafasi mbalimbali kwa tiketi ya chama hicho, hali iliyotoa majibu ya mapema juu ya jinsi matokeo yatakavyokuwa.
Kwa kuwa Rais Martin Wela katika kipindi chote cha uongozi wake alikuwa na desturi ya kufanya ziara za mara kwa mara mpaka vijijini, hakupata shida wakati wa kampeni kwani tayari alikuwa akivijua vijiji karibu vyote.
Kila alipokuwa akipita na wagombea wenzake, wananchi walikuwa wakimpokea vizuri na kumuona kama mkombozi wao kwani ndani ya kipindi kifupi tu alichokaa madarakani, aliweza kuleta mapinduzi makubwa ya kiuchumi, tofauti na waliomtangulia ambao licha ya kukaa kwa miaka mingi, hakuna chochote cha maana walichokifanya.
Kampeni ziliendelea kila sehemu, umaarufu wa chama hicho ukazidi kuwa mkubwa huku maelfu ya wananchi wakijiandikisha na kupewa kadi za chama hicho. Baada ya kuzunguka karibu nchi nzima, Rais Martin alihitimisha kampeni za chama chake kwenye Jiji la Katwe ambalo ndiyo lilikuwa makao makuu ya nchi hiyo.
Viwanja vya Nyika ambavyo mara kwa mara ndivyo vilivyokuwa vinatumika kwenye mikusanyiko mikubwa ya watu, siku hiyo vilionekana kutotosha kutokana na jinsi watu walivyokuwa wengi.
Hata spika kubwa zilizofungwa kila sehemu, zilionekana kutokidhi mahitaji ya watu wote, wagombea mbalimbali wa chama hicho wakawa wanahutubia kwa zamu na mwisho kabisa, alipanda Rais Martin Wela ambaye kabla hata hajasema chochote, umati wote ulilipuka kwa shangwe, nderemo na vigelegele, huku kila mmoja akilitaja jina lake.
Alichokuwa anakiona mbele ya macho yake, kilisababisha atokwe na machozi ya furaha kwani licha ya kukubalika sana sehemu zote alizopita kufanya kampeni, hakuwahi kudhani kwamba wananchi wa Sangabuye, hasa wakazi wa Jiji la Katwe walikuwa wakimkubali kiasi hicho.
Moyoni akajihisi kuwa na deni kubwa la kuhakikisha anayabadilisha kabisa maisha ya kila mmoja. Hata alipoanza kuhutubia, kila baada ya kuzungumza kidogo, watu walikuwa wakishangilia mno. Mpaka anahitimisha hotuba yake, bado wananchi walikuwa na shauku ya kuendelea kumsikiliza.
Mkutano ukaahirishwa huku kila aliyehudhuria akiahidi kukipigia chama cha SADT kura na kumchagua Martin Wela kuendelea kuiongoza nchi hiyo. Hatimaye kampeni zilifungwa rasmi, Martin akarudi kutulia na familia yake kwani kwa kipindi chote hicho, alikosa muda wa kukaa na mkewe na mwanaye.
“Pole sana mume wangu, najua ni kwa jinsi gani umechoka,” alisema mkewe, Sophia baada ya mumewe kurejea, akamkumbatia kwa furaha na kumpeleka mpaka kwenye chumba cha mtoto wao ambaye alikuwa amelala baada ya kulishwa chakula cha usiku.
“Kila siku anazidi kuwa mkubwa, nawapenda sana wewe na mwanangu,” alisema Martin na kwenda kumbusu mwanaye kwenye paji la uso.
“Tunakupenda pia baba, anakua haraka kwa sababu anajua nimekuahidi kumletea mdogo wake siku chache zijazo,” alisema Sophia na kumkumbatia tena mumewe, wakamwagiana mabusu kisha wakarudi chumbani kwao kupumzika, huku Sophia akiendelea kumsisitiza mumewe kwamba lazima amzalie mtoto mwingine wa kike haraka iwezekanavyo.
Hatimaye ile siku iliyokuwa ikisubiriwa kwa hamu kubwa, ya uchaguzi wa rais, wabunge na madiwani iliwadia. Wananchi wengi wa Sangabuye walijitokeza kwa wingi kwenye vituo vya kupigia kura. Foleni ndefu za watu waliokuwa wamejipanga tangu alfajiri, zilionekana kwenye
vituo vyote vya kupigia kura.
Kwa mara ya kwanza uchaguzi wa kidemokrasia ukafanyika tangu jeshi lilipoipindua nchi hiyo, wananchi wote waliokuwa na sifa za kupiga kura wakaitumia vizuri nafasi hiyo.
Mpaka ilipotimu saa sita za usiku, zoezi hilo lilifungwa baada ya kuwa watu wote wameshapiga kura.
Zoezi la kuhesabu kura lilianza haraka chini ya ulinzi mkali wa askari wa kawaida na wanajeshi waliokuwa wakipita kila sehemu kuhakikisha amani na utulivu vinadumishwa. Mpaka alfajiri ya siku ya pili ilipowadia, tayari baadhi ya vituo vilikuwa vimekamilisha zoezi la kuhesabu kura.
Chama cha SADT kilianza kung’ara tangu kwenye matokeo ya awali ambapo wagombea wake wengi wa nafasi za udiwani na ubunge waliwazidi kwa mbali wapinzani wao kutokana na wingi wa kura.
Yote tisa, kumi ilikuwa ni kwenye nafasi ya urais ambapo kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi hiyo, Martin Wela alikuwa akiongoza kwa zaidi ya asilimia tisini ya kura zote zilizopigwa.
Zoezi liliendelea kwa siku mbili mfululizo na baada ya siku ya tatu, Tume ya Uchaguzi ya Sangabuye (SEC) ikatangaza rasmi matokeo ya urais ambapo Martin Wela alishinda kwa kishindo baada ya kupata asilimia tisini na tatu ya kura zote.
Shangwe, nderemo na vigelegele vikawa zinasikika kila kona ya nchi hiyo, huku waangalizi wa uchaguzi huo kutoka mataifa mbalimbali, wakishangazwa na jinsi Martin Wela alivyokuwa akikubalika miongoni mwa wananchi wake.
Je, nini kitafuatia? Usikose Jumatatu kwenye Ijumaa Wikienda.

Comments

Popular posts from this blog

TUMIA SMS HIZI KUBORESHA PENZI LENU

FAIDA TISA ZA MBEGU ZA MABOGA KATIKA MWILI WA BINADAMU

UMUHIMU WA KUJIFUNZA SAIKOLOJIA